Thursday, November 29, 2012

AINA NNE ZA WATU...

NI imani yangu kuwa, si wote wanafahamu kwa undani aina nne za watu katika ulimwengu wa mafanikio, jambo ambalo naamini linachangia kwa kiasi kikubwa kuwafanya hawa wafanikiwe kimaisha na wengine wasifanikiwe kabisa.

Kwenye ulimwengu wa mafanikio binadamu wamegawanyika katika makundi manne ambayo ni WATENDA USAHIHI, WANAOLIDHIKA, WANAOTAKA KUPENDWA NA WASHINDI. Naomba tufuatane katika kuangali kwa undani aina hizi za watu ili kuanzia leo kila mtu afahamu yupo kundi gani.

WATENDA USAHIHI: 
Ni watu ambao katika maisha yao huwa hawataki kukosea au kuonekana wayafanyayo si sahihi. Watu wa aina hii huwa ni wagumu sana kufanya jambo ambalo akili zao hazihakiki kuwa litamalizika kwa mafanikio.Kikwazo kikubwa kwa watu wa aina hii mara nyingi ni kusitasita katika kuamua. Ni watu wa kuogopa macho ya watu hasa suala la kushindwa kutimiza malengo linapowajia akilini. Kinachowaogopesha zaidi watu wa kundi hili ni kuabika mbele za watu jambo fulani likiwaharibikia.

WANAORIDHIKA:
Kundi jingine la watu katika ulimwengu wa mafanikio ni wale wanaoridhishwa na hali zao na kwamba hawahitaji mabadiliko ya aina yoyote kwenye maisha yao. “Ndugu yangu, hali hii tumeizoea, mwaka wa nne.” Wamezoea maisha magumu.Hata hivyo, wapo wanaozoea kazi na majukumu yao ya kila siku kiasi kwamba hawataki kubadilika, hawapendi kuongezeka zaidi ya hapo walipo. Utakuta uwezo wa mfanyakazi alioanza nao miaka 7 iliyopita ni huohuo mpaka leo. Wafanyakazi wengine wanaweza kuajiriwa nyuma yake wakajitahidi kusoma, kujifunza kazi na kupanda vyeo na kumwacha mridhikaji yuko palepale. Kundi la wanaoridhika.

WANAOTAKA KUPENDWA:
Kuna watu katika maisha yao wanataka kumfurahisha kila mtu kwa lengo la kuvuta upendo wa wanadamu wenzao. Utakuta maisha yao yote ni kuwatumikia wengine kutoa fedha za maendeleo kwa kumsaidia huyu na yule kwa malipo ya kupendwa na jamii.Ni wazi kuwa watu wanaoishi katika kundi hili hawawezi kufanikiwa kwa sababu kipato chao kingi hukitumia katika kuwafanya watu wengine wafurahi na si kusukuma mbele maisha yao ya kila siku.

WASHINDI:
Kundi la mwisho la watu ni wale ambao katika maisha yao ya kila siku hupenda kufika kwenye kilele cha mambo yote wanayofanya. Hutamani kufanikiwa zaidi na zaidi, hawakubali jambo liwashinde, kila walichokusudia kukifanya huhakikisha kwamba wanakabiliana na changamoto zote na mwisho wa safari kupata ushindi.

Baada ya kuangalia hayo, ni vema kujiuliza; Je ni sahihi kutokuwa makini katika mambo yako ama kuridhika na mafanikio uliyoyapata? Inawezekana kweli mtu akaacha kusaidia wenzake kwa hofu ya kuwa katika kundi la tatu? Jibu ni hili:

Ni vema mambo matatu ya mwanzo yakaongozwa na la nne yaani USHINDI. Kwa maana hiyo kila mmoja wetu lazima awe mtu ambaye anatamani sana kufanikiwa katika maisha yake ya kila siku. Watu wote wakiwa na nia hii wataweza kuyapita makundi mengine matatu kwa uangalizi mkubwa.Hawatakubali wawe makini wasifikie malengo, hawataacha kujaribu bahati kwenye mambo ambayo akili zinaona ni magumu, hawataridhishwa na mafanikio au hali walizonazo na hawatakubali kutumika kama kuwafurahisha watu bali kila kitu watafanya kwa kiasi kwa lengo la kufika katika mafanikio sahihi.

Haya dunia yako, chaguo ni lako.


No comments:

Makaya's Forum: ISHI NA YAKO

Makaya's Forum: ISHI NA YAKO : Watakwambia unabahati kwakile ulichokifanya kilichokufanya uwepo hapo,kujipa ufalme na kuzungumzia maisha...