Tuesday, November 27, 2012

KWA NINI KUACHANA?



Matatizo yanayochangia watu kuachana yako mengi, ambayo mtu unaweza kujaza vitabu kuyaelezea, lakini uchunguzi unaonesha kuwa wapenzi huachana kutokana na udhaifu wa sababu zilizowasababisha kupendana. Kwa mfano wapenzi ambao wakati wa kupendana kwao walitamaniana kwa maumbo, sura, mvuto wa kingono na pesa huwa katika hatari ya kuachana baada ya vitu vilivyowasukuma kupendana kupoteza mvuto.

Hakuna asiyefahamu kuwa watu hubadilika tabia, umbo, sura, hufirisika na hata kutovutia tena! Hivyo mtu anapopenda kwa sababu hizo, ukomo wake huwa ni baada ya alichopenda kuondoka. Ukipenda kwa tamaa ya ngono ukishashibishwa nayo hutakuwa na sababu ya kumpenda mpenzi wako, matokeo yake utamwacha.Ukiwa umeamua kumpenda dada fulani kwa sababu anavutia, kumbuka kuwa anaweza kupata ajali akapoteza mvuto au akazeeka. Je umeshajiuliza swali itakuwaje kama mpenzi wako atapata makovu, utafanyaje baada ya mvuto wake wa usichana kuisha, nini kitafuata baada huyo mwanaume unayemsifia kwa tendo la ndoa atakapofikia ukomo wa kukutosheleza? Nadhani ni kuachana.

Sababu nyingine inayochangia wapenzi kuachana ni kutojali changuo sahihi kulingana na jinsi mtu mwenyewe alivyo.Mimi niliwahi kusoma katika Biblia Mungu akiweka wazi namna alivyozingatia kumuumbia mke Adamu kwa kusema, alimuumba mtu wa kufanana naye. Hivyo ni busara kupata mpenzi wa kufanana na wewe kwa tabia na mambo mengine ya msingi, bila hivyo mapenzi hayawezi kudumu.Kwa mfano kama wewe ni mtu wa imani kali, inakuwaje unakwenda kupendana na mpagani, huoni hicho kitakuwa kikwazo cha penzi lenu? Kwa msingi huo, lazima kupendana kuambatane na kufanana elimu, mtazamo na hata tamaduni, hii itasaidia kuondoa vikwazo vya mapenzi kuvunjika.

Lakini jambo jingine linalowafanya wapenzi wengi kuachana ni kutojali au kutofahamu kanuni za kutunza penzi. Kuna watu wanaweza kuchaguana kwa kuzingatia maelekezo yote, lakini wakajikuta wanaachana kwa kutojua namna ya kukuza na kudumisha upendo wao.

Nasema hivyo kwa sababu, kumpata mpenzi ni jambo jingine na kumtunza ni hatua nyingine ambayo ni ya msingi. Inawezekana kabisa ukampata wa kufanana naye, lakini ukajikuta unashindwa kudumu naye kwa sababu ya kumuudhi mara kwa mara tena kwa kusudi, kumnyanyasa, kusikiliza umbea, wivu, kutomjali na kumpuuza.Kinachosikitisha sana katika mapenzi ni kuona watu wanawapata wapenzi wa kweli, badala ya kufurahika nao wanawachezea kwa kufanya vurugu na kuwa waanzilishi wa usaliti na ujeuri. Ushauri wangu ni kuwa, ukipata wa kukupenda usimchezee, mtunze na umuonyeshe kweli kuwa wewe ni wa kufanana naye.

Mwisho, mapenzi lazima yakose sababu, ukiulizwa unampendea nini mpenzi wako? Jibu liwe sijui, kwani ukitaja sababu yoyote unakuwa katika hatari ya kuachana kwa vile kila sababu ina mwisho wake. Penzi ni lidhiko la moyo lisilokuwa na kwa nini. Ukisema nampenda kwa sababu ananijali, asipokujali, ukisema ni mzuri akiwa mbaya, ana pesa akiishiwa, mtundu,..uwanjani akichoka? Bila shaka penzi nalo litachoka!

No comments:

Makaya's Forum: ISHI NA YAKO

Makaya's Forum: ISHI NA YAKO : Watakwambia unabahati kwakile ulichokifanya kilichokufanya uwepo hapo,kujipa ufalme na kuzungumzia maisha...